Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Waziri Mhagama aiogonza OSHA kukabidhi Tuzo kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mhe. Jenista Mhagama, kwa niaba ya serikali, kupitia Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), ameikabidhi Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Tuzo yenye lengo la kutambua mchango wa kamati hiyo katika kuboresha utendaji wa Wakala hiyo.

Waziri Mhagama ameikabidhi kamati hiyo tuzo leo tarehe 29 Machi, 2021 jijini Dodoma wakati kamati hiyo ilipokuwa ikipokea taarifa ya utekelezaji wa Wakala hiyo. Amebainisha kuwa ushauri wa kamati hiyo umeiwezesha wakala kuboresha Utendaji kwa kutengeneza mifumo ya kimtandao ya kurahisisha utendaji wa Wakala hiyo, Kupunguza tozo saba zilizokuwa kero kwa wadau wa OSHA pamoja na kuongeza mapato ya Wakala hiyo.

“Mara nyingi tumezoea serikali kupewa tuzo kwa kufanya vizuri lakini tumekuwa tukisahau kuwa kuna baadhi ya walioisaidia serikali kufanya vizuri. Tumepima utekelezaji na utendaji wa OSHA katika kuzingatia ushauri wenu, tumeona kwa sasa hata gawio limeendelea kuongezeka linalotolewa na OSHA kwenye serikali, mifumo ya kimtandao imetengenezwa ya kurahisisha utendaji lakini pia tozo saba zimefutwa, hivyo hatunabudi kuwashukuru kwa mchango huo umeiboresha OSHA” Amesema Mhe. Mhagama.

Tozo saba ambazo OSHA tayari imezifuta kufuatia ushauri uliotolewa na Kamati hiyo ni; Tozo ya Usajili wa maeneo ya kazi, Tozo ya Fomu ya Usajili, Tozo ya ada ya leseni ya kukidhi matakwa ya sharia ya Usalama na Afya Mahali Pa kazi, Tozo ya Ushauri wa mambo Usala na Afya, Faini zinazohusiana na vifaa vya kuzimia moto, Tozo ya elimu kwa umma, Tozo ya Uchunguzi wa ajali ambayo imepunguzwa kutoka shilingi 500,000/= hadi shilingi 120,000/=.

Akiongeoa baada ya kupokea Tuzo hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, Mhe. Mohamed Mchengerwa amefafanua kuwa kamati hiyo imekuwa ikitoa ushauri kwa OSHA wa namna ya kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu pamoja na kuongeza kipato. Aidha, amebainisha kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu inayoirtaibu Wakala hiyo, imekuwa sikivu kwa kufuata ushauri wao wa kufuta tozo ambapo kwa kiasi kikubwa imekuwa ni faraja kwa watanzania na wawekezaji nchini.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana na Ajira) Mhe. Patrobas Katambi, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Wenye Ulemavu) Mhe. Ummy Ngeriananga, Katibu Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Andrew Massawe, Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda, pamoja na baadhi ya Wakurugenzi wa OSHA.

OSHA ni Wakala wa serikali chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na wenye Ulemavu). Taasisi hii ina wajibu wa kuwalinda wafanyakazi dhidi ya vihatarishi vilivyopo katika sehemu za kazi ambavyo vinaweza kusabisha magonjwa na ajali. Wajibu huu unatekelzwa kupitia usimamizi wa Sheria Na. 5 ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi ya mwaka 2003.

Mwaka 2001, ilianzishwa OSHA chini ya Sheria Na. 30 ya Wakala wa Serikali ya mwaka 1997 kama sehemu ya Mpango wa Maboresho katika utoaji wa Huduma za Serikali kwa wananchi. Makusudi ya kuanzishwa kwa OSHA ni kupata chombo cha serikali kwa ajili ya kusimamia Usalama na Afya mahali pa kazi. OSHA ina jukumu la kuhakikisha kuwa wafanyakazi wanafanya kazi katika mazingira ambayo ni salama na yenye kulinda afya zao kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa katika kuzuia ajali na magonjwa yatokanayo na kazi.