Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Wastaafu waaswa kuzingatia nidhamu ya fedha baada ya kustaafu


Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kupitia Kitengo cha Ukuzaji Tija imetoa mafunzo ya kujiandaa na maisha baada ya kustaafu kwa watumishi wanaotarajiwa kustaafu na kuwaasa kuwa na nidhamu ya fedha na waangalifu kwenye miradi watakayowekeza.

Akifunga mafunzo hayo ya siku tano kwa watumishi hao kutoka Takukuru, Dawasa, Rita, Feta na Chuo cha Ustawi wa Jamii, Novemba 17, 2023 Mjini Morogoro, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali wa Ofisi hiyo, Leonard Mchau amesema watumishi wanapostaafu wamekuwa wakihamasishwa kutumia mafao yao kuwekeza kwenye miradi isiyo na tija na kusababisha mafao kupukutika.

Aidha Mkurugenzi Mchau ameipongeza Serikali ya awamu ya Sita Chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa kipaumbele kwa Wastaafu kupata fursa ya kupata mafunzo hayo yenye kaulimbiu ‘Kustaafu Sio Mwisho wa Maisha.’

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ukuzaji Tija wa Ofisi hiyo, Yohana Mdadi ameeleza kuwa kitengo hicho kina wajibu wa kutoa na kuratibu mafunzo hayo na kuwashukuru wastaafu kwa kushiriki kupata elimu muhimu ya kujiandaa kustaafu.

Naye, Mshiriki kutoka DAWASA, Poncean Muyaga ameishukuru serikali kwa kuwezesha kupata mafunzo hayo na kwamba elimu waliyoipata itawasaidia kuondoa hofu na kujiandaa katika uwekezaji wenye tija.