Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Prof. Ndalichako: Walimu Tarajali Kuanza Kufundishwa Lugha ya Alama


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Prof. Joyce Ndalichako, amesema serikali ya awamu ya sita imedhamiria kutatua changamoto ya mawasiliano kwa viziwi na kuanzia mwaka 2024 walimu wote tarajali watafundishwa lugha ya alama ili kuwa na wataalamu wa kutosha.

Akizungumza leo Septemba 30, 2023 jijini Mbeya kwenye kilele cha wiki ya Viziwi kitaifa, Prof.Ndalichako amesema katika mapitio ya sera mpya ya elimu serikali itatatua kabisa changamoto ya upungufu wa walimu wa lugha ya alama kwa kuwa walimu wote tarajali watakuwa wanafundishwa lugha ya alama na itakuwa somo la lazima.

Waziri Ndalichako amesema serikali imewatambua walimu 102 wa lugha ya alama na kati yao 88 wapo shule za msingi na 24 wapo kwenye shule zisizo na viziwi hivyo utaratibu unafanyika wa kuhakikisha walimu hao wanapelekwe kwenye shule zenye viziwi.

Aidha, amesema tayari imefanya mafunzo ya lugha ya alama kwa watoa huduma watatu kwa kila hospitali ya rufaa ili kupunguza vikwazo kwenye upatikanaji wa huduma za afya na imejipanga kufikia Hospitali za Wilaya na vituo vya afya.

Amebainisha kuwa katika mwaka wa fedha 2023/24 serikali imetenga Sh.Bilioni 4.2 kwa ajili ya kununua vifaa saidizi kwa watu wenye mahitaji maalum ikiwamo kununua vifaa vya kufundishia lugha ya alama.

Naye, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Ummy Nderiananga ameiasa jamii kuendelea kuunga mkono juhudi zinazofanywa na watu wenye ulemavu katika jamii zetu kwa kuwashirikisha kikamilifu katika shughuli zote za uzalishaji mali.

Kwa upande wake, Spika wa Bunge, Mhe. Dkt. Tulia Ackson amesema kuwa, Bunge lipo tayari kuunga mkono jitihada mbalimbali zinazofanywa katika kuhakikisha wenye ulemavu wanafanya kazi zao kwenye mazingira rafiki kwa kuboresha sheria.

Akisoma risala, Mjumbe wa Bodi ya Utendaji kutoka Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA), Subira Upurute ameipongeza serikali namna inavyoendelea kutatua changamoto wanazokabiliana nazo ikiwamo ya uhaba wa wakalimani wa lugha ya alama kwenye upatikanaji wa huduma za afya na elimu.