Tanzania emblem
The United Republic of Tanzania

Prime Minister's Office

Labour, Youth, Employment and Persons with Disability

News

Katambi aipongeza TANESCO kwa mpango wa kuwaendeleza Vijana Vyuo Vikuu


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi ameipongeza TANESCO kwa kuanzisha programu mahususi ya kuwatambua, kuwasaidia na kuwaendeleza vijana waliopo Vyuo Vikuu wanaosoma fani ya uhandisi kupitia mpango wa “Graduate Trainee”.

Mhe. Katambi amebainisha hayo Desemba 12, 2023 Jijini Dodoma katika Ufunguzi wa Baraza Kuu la 53 la Wafanyakazi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) ambapo amesema mpango huo utaongeza idadi ya wataalam wa uhandisi wazalendo kutekeleza miradi inayotekelezwa na Mhe. Rais Samia.

Aidha, amempongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutekeleza mradi mkubwa wa kuzalisha umeme wa maji wa Julius Nyerere ambao utakuwa na uwezo wa kuzalisha Megawati 2115 ambapo mradi huo umefikia asilimia 94.

Amesisitiza Ofisi hiyo kupitia Kamishna wa Kazi itaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwa kutoa vibali vya kazi kwa wataalamu wa kigeni wanaoajiriwa katika miradi ya umeme ili ikamilike kwa wakati.

“Niwapongeze kwa jitihada mnazoendelea kuzikuchukua kuhakikisha Mradi wa Kuzalisha Umeme kwa nishati ya jua uliopo Kishapu Mkoani Shinyanga unaanza, ambapo utakapokamilika utatupatia takribani Megawati 150 za umeme na hivyo kuongeza kiwango cha upatikanaji wa umeme nchini”

Sambamba na hayo ametoa rai kwa TANESCO kuongeza jitihada za kuwaelimisha wananchi kuhusiana na hatua wanazozichukua katika kukabiliana na upungufu wa umeme na kutoa taarifa juu ya kukosekana kwa umeme.